|
Wakati dirisha dogo la usajili
linafungwa leo Saa 6:00 usiku, klabu ya
Yanga SC inafikiria kumuacha Mbrazil mmoja kati ya Andrey Coutinho na Emilson de Oliviera Rogue, ili
imrejeshe Mganda Hamisi Kiiza, au isajili mchezaji
mwingine.
Kiiza aliondoka kambini siku moja
kabla ya mechi ya Nani Mtani Jembe
ambayo Yanga SC ilifungwa 2-0 na Simba SC Jumamosi Uwanja wa Taifa, Dar es
Salaam kufuatia taarifa kwamba yeye ndiye atakayekatwa baada ya kusajiliwa Mliberia,
Kpah Sean Sherman.
Lakini uongozi wa Yanga SC
unasistiza bado haujamuacha mchezaji huyo,
ingawa taarifa zinasema alikwenda kujaribu kujiunga na mahasimu, Simba SC ambako alikwama kwa sababu
hakuwa na barua ya kutemwa na bado ana Mkataba na mwajiri wake wa sasa.
Kutemwa Kiiza ni pendekezo la kocha Mbrazil wa Yanga SC, Marcio Maximo, lakini uongozi wa klabu hiyo hadi sasa haujaafiki.
Kiiza aliondoka kambini kabla ya mechi ya nani mtani jembe. |
Yanga SC hawajaridhishwa na uwezo
wa Coutinho, aliyeichezea klabu hiyo
mechi 11 na kuifungia mabao matatu, lakini kikwazo ni Mkataba wake mrefu ambao utawalazimu kumlipa fedha
nyingi wakimuacha.
Wakala aliyemleta Mliberia,
Sherman ambaye amewavutia wana Yanga wengi
baada ya kuichezea klabu hiyo kwa mara ya kwanza juzi, amewahakikishia viongozi wa klabu hiyo anaweza
kuwapatia mchezaji mwingine mzuri ndani ya Saa 12 na kukamilisha usajili wake
wote.
Katika dirisha dogo, Yanga SC
imesajili wachezaji watatu mbali na Mbrazil
Emerson na Mliberia Sherman, mwingine ni mzalendo mshambuliaji Dan Mrwanda.
Kwa upande wa Simba SC, jana
imewasainisha mikataba wachezaji wawili
wa kimataifa wa Uganda, beki Juuko Murushid na mshambuliaji Simon ‘Sam’ Sserunkuma, siku moja baada ya
kuisaidia timu hiyo kushinda 2-0 dhidi ya Yanga SC.
Wawili hao wote walicheza juzi
mechi ya Nani Mtani Jembe, Simba SC ikiwafunga
mahasimu wao wa jadi, Yanga SC 2-0 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam mabao ya kipindi cha kwanza ya
Awadh Juma na Elias Maguri.
Wawili hao wanachukua nafasi za
Warundi kiungo Pierre Kwizera na mshambuliaji
Amisi Tambwe wanaotemwa na sasa wanaungana na Waganda wenzao, beki Joseph Owino na washambuliaji Dan
Sserunkuma na Emmanuel Okwi kukamilisha
idadi ya wachezaji watano wa kigeni kwa mujibu
wa kanuni za Ligi Kuu.
Tambwe mfungaji bora wa ligi kuu bara msimu uliopita. |
Tambwe aliyejiunga na Simba SC
msimu uliopita pamoja na Mrundi mwenzake,
Gilbert Kaze aliyetemwa Desemba mwaka jana, anaondoka Msimbazi baada ya kuichezea timu hiyo mechi 43
na kuifungia mabao 26.
Tambwe ndiye aliyeibuka mfungaji
bora wa Ligi Kuu ya Bara msimu uliopita-
baada ya kuivutia Simba SC akiichezea Vital’O ya Burundi katika Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati,
maarufu Kombe la Kagame nchini Sudan mwaka jana na
kuiwezesha kutwaa taji hilo naye akiwa
mfungaji bora.
Pierre Kwizera aliyesajiliwa kutoka
Ivory Coast mwanzoni mwa msimu, hadi
anaondoka amecheza mechi 14 bila kufunga bao.
Kwa upande wa Azam FC, imeongeza
wachezaji watatu karika dirisha dogo,
ambao ni beki Serge Wawa Pascal raia wa Ivory Coast aliyekuwa anacheza El Merreikh ya Sudan, winga
wa Uganda Brian Majwega aliyekuwa
anacheza KCCA ya Kampala na kiungo mzalendo, Amri Kiemba aliyetua kutoka Simba SC.
Wawa na Majwega wanaungana na
pacha wa Ivory Coast, Kipre Tchetche na
Kipre Balou na Mrundi, Didier Kavumbangu kukamilisha idadi ya wachezaji watano wa kigeni Azam FC, huku
Leonel Saint- Preux wa Haiti akitemwa.
Fahamu kuwa Azam FC inaridhika na
uwezo wa Leonel kiuchezaji, lakini
nidhamu yake mbovu ambayo alikuwa amekwishaanza kuwaambukiza wachezaji wengine waadilifu wa
klabu hiyo, inafanywa aachwe.
Habari kutoka ndani ya Azam FC zinasema
kwamba Leonel alikuwa mfano mbaya ndani
ya kambi ya timu na alikwishaanza kuwaambukiza na wachezaji wengine tegemeo wa
timu hiyo.
Tayari Azam FC imekwishaziba
pengo la Mhaiti huyo kwa kumsajili winga
wa kimataifa wa Uganda, Brian Majwega.
Winga huyo wa KCCA ya Kampala,
Uganda alisaini Mkataba wa miaka miwili
jana mjini Kampala, Uganda kujiunga na mabingwa hao wa Tanzania Bara.
Majwega anakuwa mchezaji wa tatu
kusajiliwa na Azam FC katika dirisha
dogo baada ya beki Serge Wawa Pascal kutoka Ivory Coast, aliyekuwa anacheza El Merreikh ya Sudan na
Amri Kiemba aliyekuwa Simba SC, ambaye amesainiwa kwa
mkopo hadi mwisho wa msimu.
Na anakamilisha idadi ya
wachezaji watano wa kigeni, baada ya Mrundi
Didier Kavumbangu na Kipre Tchetche, Kipre Balou na Serge Wawa wote kutoka Ivory Coast.
Majwega anatarajiwa kuanza
mazoezi na kikosi cha Azam FC leo mjini Kampala,
chini ya makocha Mcameroon Joseph Marius Omog na Mganda George ‘Best’ Nsimbe ambacho kipo kambini
mjini humo tangu Ijumaa hadi Desemba 22,
mwaka huu.
Kwa upande wa Vinara wa Ligi Kuu hadi sasa, Mtibwa Sugar
wao wameimarisha kikosi chao kwa kumsajili mkongwe, Nahodha wa zamani wa timu ya taifa ya Tanzania, kiungo Henry Joseph Shindika aliyewika
Simba SC kabla ya kwenda Norway.
Zaidi ya hapo, Wakata Miwa hao wa
Manungu wameendelea na utamaduni wao wa
kupandisha wachezaji chipukizi kutoka timu yao ya vijana.
Mbeya City imeimarisha safu yake
ya ulinzi kwa kumsajili beki mkongwe,
Juma Said Nyosso, wakati Coastal Union imemsajili kiungo Abdulhalim Humud ‘Gaucho’.
Lakini pia zipo taarifa kuwa
Kiungo wa zamani wa Simba, Haruna Moshi
‘Boban’, anatarajia kumalizana na Friends Rangers leo.
Boban anatarajiwa kujiunga na friend Rangers. |
Friends Rangers ya daraja la kwanza imekuwa ikipambana kupanda ligi kuu.
Katibu Mkuu wa Friends Rangers,
Herry Mzozo amesema wameshafanya mazungumzo
na Boban na wako katika hatua nzuri.
Boban amekaa msimu mzima bila ya
kuichezea timu yoyote.
Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) linatarajiwa kutoa orodha kamili ya wachezaji waliongia katika klabu zote kwenye dirisha hili dogo baada ya Saa 6:00 usiku wa leo.
0 comments:
Post a Comment